Serikali imewahimiza wafanyabiashara na wazalishaji nchini kutumia kikamilifu fursa za masoko ya kikanda na kimataifa ili kuongeza mauzo ya nje ili kuvutia wawekezaji na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.
Hayo yameelezwa leo jijini Dar es Salaam na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara, Aristides Mbwasi wakati wa Mkutnao wa wadau kuhusu kutumia fursa ya kuuza bidhaa katika soko la China bila ushuru (Zero Tariff) ulioandaliwa na wizara hiyo kwa kushirikiana na Jamhuri ya Watu wa China- Tanzania.
Akizungumza katika mkutano huo, Mbwasi amesema Tanzania inanufaika na mifumo mbalimbali ya biashara ikiwemo ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA) pamoja na fursa nyingine kutoka kwa washirika wa kimataifa kama China.
Amesema fursa hizo zinawezesha bidhaa zinazozalishwa nchini kuingia katika masoko makubwa hatua inayoongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania kimataifa.
Hata hivyo, ameeleza kuwa bado kuna changamoto zinazokwamisha matumizi kamili ya fursa hizo, ikiwemo uelewa mdogo wa wafanyabiashara kuhusu taratibu za biashara za kimataifa, changamoto za ubora wa bidhaa, gharama za usafirishaji pamoja na ukosefu wa taarifa sahihi za masoko.
Amesema ili kutatua changamoto hiyo ni umuhimu kuendelea kuwapo kwa ushirikiano kati ya serikali, sekta binafsi na taasisi zinazoshughulikia biashara ili kuhakikisha wafanyabiashara wa Tanzania wanatumia kikamilifu fursa za kuuza bidhaa nje ya nchi.
Aidha Mbwasi ameitaja China kuwa moja ya soko kubwa na muhimu kwa bidhaa za Tanzania kutokana na ukuaji wa uchumi wake na mahitaji makubwa ya bidhaa mbalimbali.
Ingawa ilibainishwa kuwa ili bidhaa za Tanzania zipate nafasi katika soko la China, ni lazima zikidhi vigezo ikiwemo kuthibitisha kuwa bidhaa hizo zimezalishwa Tanzania kwa asilimia 100 au zimefanyiwa uchakataji wa kutosha hapa nchini.
10YrsJembefm #Familiamoja #AhsantekwaTime